Uingereza na Marekani zinaamini kuwa Iran ilifanya shambulio la meli ya mafuta ambalo liliwauwa watu wawili, na zimeapa kujibu shambulio hilo, zikilitaja kuwa ni ukiukaji wa sheria ya kimataifa.
Meli hiyo MV Mercer Street, ya kampuni inayomilikiwa na Israel , ilishambuliwa ilipokuwa kwenye mwambao wa Oman siku ya Alhamisi.
Raia wa Uingereza na mwingine wa Romania waliokuwemo ndani yake waliuawa.
Taarifa hii inakuja baada ya Waziri Mkuu wa Israeli Naftali Bennett kusema kuwa kulikuwa na "ushahidi" kwamba adui wa muda mrefu Iran alihusika.
Bw Bennett alionya kwamba " tunajua jinsi ya kutuma ujumbe kwa Iran kwa njia yetu wenyewe", huku Iran ikikana kile ilichokiita "shutuma zisizo na msingi".
Shambulio dhidi ya MV Mercer Street linaonekana kuwa ni la hivi karibuni katika ''vita vya kimkakati'' vinavyoendelea ambavyo havijatangazwa baina ya Israeli na Iran.
Tangu mwezi Machi kumekuwa na mashambulio kadhaa dhidi ya meli za nchi zote mbili mbili Israeli na Iran. Waathiriwa katika matukio hayo huwa ni nadra.
Iran pia imeishutumu Israeli kwa kulenga viwanda vyake vya nyuklia na wanasayansi wake.
Katika taarifa iliyotolewa Jumapili, Waziri wa mambo ya nje wa Uingereza Dominic Raab alisema kuwa Uingereza inaamini kuwa Iran ilitumia moja ya ndege zake zisizo na rubani katika shambulio hilo dhidi ya meli ya MV Mercer Street, ikilitaja kuwa la "makusudi'', na kwamba ni ukiukaji wa wazi wa sheria ya kimataifa ".
"Iran lazima iache mashambulio ya aina hii, na meli lazima ziruhusiwe kusafiri kwa uhuru ,"aliongeza.
Waziri wa mambo ya nje wa Marekani Antony Blinken alisema kuwa Washington pia "inaamini kwamba Iran ilifanya hili ",na kwamba "jibu linalofaa" litafuatia.
Waziri mkuu wa Israeli alisema kuwa anatarajia jamii ya kimataifa kuwa wazi na kuiambia Iran imefanya kosa baya.

No comments:
Post a Comment