Search This Blog

Friday, August 20, 2021

Kiduku, Dulla Mbabe kuonyeshana ubabe leo


Pambano la ngumi lililokuwa linasubiriwa kwa hamu na mashabiki wa masumbwi, kati ya Twaha Kiduku na Dulla Mbabe hatimaye limefika baada ya wababe hao kupima uzito jana Agosti 19, tayari kwa kupanda ulingoni leo.

Mchezo huo umezidi kuvuta hisia za mashabiki wengi kutokana na uwepo wa zawadi ya gari aina ya Crown ambayo atapewa mshindi.

Wakitambiana baada ya kumaliza kupima uzito Ubungo Plaza, jijini Dar es Salaam ambapo pambano litapigwa, kila mmoja amepania kummaliza mpinzani wake mapema na kuondoka na gari hiyo.

Mabondia hao wenye majina makubwa katika ngumi za kulipwa kwa sasa, watapigana raundi 10, uzito wa Super Middle.

"Nimefanya mazoezi ya kutosha, najiamini na ninapenda kumwambia kaka yangu Dulla kuwa kama amejiandaa na mimi nimejiandaa, shoo shoo, sina maneno mengi," ametamba Kiduku.

Akijibu maneno ya Kiduku, Dulla Mbabe amesema:"Leo imepita tukutane kesho ulingoni, atakufa mtu kesho,".

Mabondia hao wanakutana kwa mara ya tatu ambapo pambano la kwanza Kiduku alishinda na la pili wakatoka sare.

Kwa upande wake muandaaji wa pambano hilo, Mkurugenzi wa Peak Time Promotion, Kapten Seleman Semunyu, amesema maandalizi ya pambano hilo yamekamilika na utakuwa ni usiku wa tofauti wenye burudani za kutosha.

Amesema uzito wa mabondia wote umetimia na wako tayari kuwapokea watanzania kutoka maeneo mbalimbali na kuwahakikishia kuwa watafurahia shoo.

"Ukiangalia hata katika zoezi la kupima uzito mambo yamekwenda vizuri na taratibu zote zimefuatwa, ulinzi utakuwepo wa kutosha, ukumbi una AC za kutosha," amesema.

Tofauti na pambano la wakali hao wawili, yatakuwepo mengine zaidi ya 10 baadhi ni Selemani Kidunda dhidi ya Paul Kamata,Cosmas Cheka na Ismail Galiatano.

Wengine ni George Bonabucha na Sunday Kiwale,Seba Temba atatwangana na Albano Clement, huku wanawake Grace Mwakamele akivaana na Felista Mwakatika.


No comments:

Post a Comment

Punguza kilo tano kwa siku saba

  NI watu wachache wanaopenda kunenepa, wengi wanapenda miili ya wastani kwa kuwa  unene si mzuri. Ukiwa mnene si tu kwamba unakaribisha m...