Umoja wa Afrika umemchagua rais wa zamani wa Ghana John Mahama kuwa mpatanishi maalum wa Somalia ili kujaribu kutatua mgogoro wa kisiasa kufuatia kucheleweshwa kwa uchaguzi.
Kulingana na taarifa ya umoja huo, jukumu la Mahama aliye na miaka 62 litakuwa kutafuta suluhisho la pamoja ili uchaguzi wa Somalia uweze kufanyika ndani ya muda mfupi ujao. Anatarajiwa kusafiri kuelekea Somalia hivi karibuni.
Mwenyekiti wa Halmashauri Kuu ya Umoja huo Moussa Faki amewahimiza viongozi wa Somalia kuingia katika majadiliano kwa nia njema ili kupata suluhu ya pamoja katika mgogoro huo wa uchaguzi.
Faki amesema Somalia inahitaji serikali iliyochaguliwa kidemokrasia iliyo na uhalali na mamlaka ya kusuluhisha changamoto nyengine za kisiasa na kikatiba zinazotishia uthabiti wa taifa hilo la pembe ya Afrika na kanda nzima.

No comments:
Post a Comment