Search This Blog

Thursday, August 13, 2020

Dkt Gwajima akerwa na utendaji wa kusua sua kwa timu ya Afya Wilaya ya Maswa

Naibu Katibu  Mkuu, Ofisi ya Rais TAMISEMI anayeshughulikia afya, Dkt. Dorothy Gwajima amemuagiza Mkurugenzi wa Halmashauri ya Maswa, Dkt. Fredrick Sagamiko  kufanya mabadiliko ya haraka kwa Timu ya Afya ya Wilaya  hiyo kutokana na kutokuwa na utendaji mzuri na kuweka watendaji wapya wenye kasi inayotarajiwa na wananchi.


Agizo hilo amelitoa leo Wilayani Maswa baada ya kufanya ziara katika hospitali ya Wilaya hiyo na kugundua timu ya afya kutotekeleza wajibu wake kwa ufasaha katika maeneo mengi licha ya kujengewa uwezo na Mkoa mara kadhaa bila kuwa na mabadiliko katika utendaji wao.


Dkt.Gwajima amefanya maamuzi hayo baada ya kuona hali ya utendaji wao katika nafasi zao kama timu ya afya ya msingi hawazitendei haki hivyo ili kutoleta madhara makubwa kwa jamii amemtaka Dkt. Sagamiko kufanya mabadiliko kwa haraka.


Aidha Dkt. Gwajima katika ziara yake amepata kukagua vitengo vyote katika hospitali hiyo na kugundua baadhi ya mapungufu katika vitengo hivyo yakiwemo hali duni ya usafi huku kukiwa na vyoo vilivyojengwa kwenye jengo jipya na badala ya kutumiwa vimefungwa na kugezwa kuwa stoo ya vitabu .


Dkt. Gwajima amesema  kuwa  Serikali  ililenga kuwajali wananchi wake, Vilevile, amekagua huduma ya vipimo vya X-ray na kubaini havitolewi kwa sababu ambazo hazina msingi kwani mashine hiyo ipo na inafanya kazi.


“Naagiza  mara moja vyoo vya nje vifanyiwe usafi na mnitumie picha kabla sijafika Dodoma na hivi vipya mlivyogeuza stoo ya vitabu vianze kutumika ndani ya saa 48”,ameagiza Dkt. Gwajima.


Wakati huo  Dkt. Gwajima amewapa masaa 24 tu huduma za vipimo vya X-ray zirejee hapa na wananchi waanze kupata huduma ya vipimo hivyo.


Pia Dkt. Gwajima amemuagiza Mkurugenzi huyo kuwa maelekezo yote na mapungufu yaliyobainika katika hospitali hiyo yawe yametekelezwa kwa ufasaha na kuwasilisha taarifa  katika Ofisi ya Rais TAMISEMI kwa siku zisizo zidi  14.


Katika hatua nyingine Dkt. Gwajima amemtaka Mkaguzi wa Ndani wa Halmashauri hiyo kukamilisha ndani ya wiki mbili taarifa ya matumizi ya dawa bila maeleezo ya wapi zilitumika ili wahusika waweze kurudisha fedha hizo na kuchukuliwa hatua za kisheria kwa kila atakaye kuwa anahusika katika sakata hilo.


“Mali ya Serikali haitumiwi bila utaratibu na bila taarifa hata siku moja , hivyo ukishindwa kuwajibika na kuanza kuiletea hasara kwa Serikali ambayo imekuajiri ili uipe ushirikiano kujenga Taifa ujue wewe ni wa kuwekwa pembeni tu hakuna namna ingine ili nafasi yako apewe mwingine mwenye kujua thamani ya kuwa mtumishi  mwenye weledi katika kuwajibika na kujali ili mali iliyopo iwanufaishe walio wengi katika Taifa”, amesisitiza Dkt. Gwajima.


Akimalizia Dkt. Gwajima amewapongeza baadhi ya watumishi katika hospitali hiyo wanaofanya majukumu yao kama inavyotakiwa akiwemo Afisa Ustawi wa Jamii Bw. Abakos kwa weledi wake katika kuelimisha jamii katika kupenda kujiunga na Bima za Afya na kupunguza wanaotibiwa kwa misamaha kwa asilimia 50.


Naye Mkurugenzi wa Halmashauri ya Maswa, Dkt. Fredirick Sagamiko amesema kuwa maagizo yote yaliyotolewa yatafanyiwa kazi kwa wakati na pale panapohitaji kuchukua hatua stahiki zitachukuliwa kwani awali kulitokea changamoto  na yeye  akafanya mabadiliko.


 “Baada ya miezi mitatu tunatamani urudi kuona utekelezaji wa maagizo uliyotoa leo na ninakuahidi kuwa mabadiliko hayo yataleta matokeo chanya katika utendaji wetu”, amesema Dkt. Sagamiko.


Kwa upande wake Mganga Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Dkt. Festo Dugange amemshukuru Naibu Katibu Mkuu kwa kuwa mwalimu mzuri ambaye amezitambua kazi zao walizofanya kwa weledi na kuwapa mbinu nyingi mpya za kufikia mafanikio ya kuleta ubora katika utendaji wao.


“Naamini kuwa kupitia mbinu hizi tutatekeleza ipasavyo na kufanya mkoa wa Simiyu kuwa kituo cha watu kuja kujifunza utendaji kazi mzuri wenye matokeo kwa wananchi”, ameeleza Dkt. Dugange.



No comments:

Post a Comment

Punguza kilo tano kwa siku saba

  NI watu wachache wanaopenda kunenepa, wengi wanapenda miili ya wastani kwa kuwa  unene si mzuri. Ukiwa mnene si tu kwamba unakaribisha m...