
Dar es Salaam. Bodi ya Ligi imewataka wadau na klabu kutoa maoni juu ya marekebisho na maboresho ya kanuni zinazotumika, baada ya kubaini mkanganyiko.
Mtendaji Mkuu Almas Kasongo, ameanza kusimamia eneo la kanuni ambalo limekuwa kaa la moto kwa klabu nchini.
Akizungumza na gazeti hili Dar es Salaam jana, Kasongo alisema wametoa fursa kwa wadau wa soka na klabu kutoa maoni kuhusu uboreshaji wa kanuni hizo.
Kasongo alisema mchakato huo umeanza mapema ili msimu ujao wa Ligi Kuu Tanzania Bara zianze kutumika baada ya kufanyiwa maboresho akitoa mfano kanuni ya kutangaza kikosi kabla ya mechi inavyowapa wakati mgumu kuisimamia.
“Tunatoa nafasi kwa wadau wa soka, wakiwemo waandishi wa habari, timu zote ili waweze kutoa maoni yao juu ya maboresho na marekebisho ya kanuni zetu ili kufanya vizuri,”alisema Kasongo.
Alisema kanuni ya kutangaza kikosi klabu inatakiwa kuwasilisha majina ya wachezaji katika kikao cha saa nne asubuhi siku ya mchezo wakati ligi za nje huwasilishwa saa moja na nusu kabla ya mchezo.
Mtendaji huyo alisema wataboresha kanuni zenye upungufu ambazo zimekuwa kikwazo kwa klabu kuzitekeleza jambo ambalo limekuwa changamoto katika usimamizi.
No comments:
Post a Comment