Search This Blog

Monday, September 13, 2021

Serikali yazidi kuimarisha miundombinu ya elimu

Watendaji wapewa wito wa kutumia rasilimali vizuri katika kusimamia ujenzi wa miradi ya maendeleo inayojengwa katika maeneo yao. Serikali imeweka matumizi ya force acount ili kusaidia thamani ya miradi ya ujenzi iendane na kiasi cha fedha zilizotolewa kwa kushirikiana na kamati ya usimamizi wa  ujenzi.

Hayo yamesemwa na Mkuu wa wilaya ya Karatu Mh. Abbas Kayanda alipotembelea ujenzi wa miundo mbinu ya elimu na kupokea taarifa ya vyumba vya madarasa katika shule za sekondari za Domel, Baray na Mang’ola kulingana na matarajio ya kupokea wanafunzi wa kidato cha kwanza. Sambamba na hilo ametembelea miradi ya ukamilishaji wa maabara katika shule ya sekondari Domel na Mang’ola . shule hizo zimepewa kiasi cha shilingi million 30 kila moja kwa ajili ya ukamilishwaji wa maabara ya somo la kemia. Mh. Kayanda ameoneshwa kuridhishwa na ujenzi wa miundo mbinu ya maabara ya sekondari hizo. Amepongeza Mkuu wa shule ya sekondari Mang’ola kwa kuweza kubaki na  kiasi cha shilingi million 4i, ambacho tayari kimeombewa kibali kwa mkurugenzi mtendaji wa Halmashauri ya Karatu kwa ajili ya kutumika  kupiga plasta katika majengo ya mabara ya fizikia na bailojia.

Mh. Kayanda ametembelea shule ya sekondari Baray ambayo serikali za vijiji vinne vinavyozunguka shule hiyo vimekubaliana kujenga na kuinua maboma mawili ya madarasa kwa ajili ya kukabiliana na upungufu wa madarasa. Mh. Kayanda amepongeza jitihada za Halmashauri ya vijiji hivyo, huku Halmashauri ya wilaya ya Karatu ikitenga katika mwaka huu wa fedha kiasi cha million 10 kwa ajili ya ujenzi wa vyumba vya madarasa.

Katika hatua nyingine Mh. Kayanda ametembelea shule ya msingi Qangnded iliyopewa kiasi cha million 40 kwa ajili ya ujenzi wa vyumba viwili vya madarasa  kupitia mfuko wa EP4R. Huku kiasi kingine cha million 19 kimetolewa kwa ajili ya ujenzi wa matundu ya vyoo katika shule hiyo. Mh. Kayanda amehimiza wakandarasi kumaliza kazi hiyo kwa mujibu ya muda ulioainishwa kwenye mkataba, na kuhakikisha ujenzi wa miundo mbinu ya vyumba vya madarasa unaendana na thamani ya fedha iliyotolewa.

Amesema lengo la serikali ni kuhakikisha mazingira ya kujifunza na kufundishia yanakuwa mazuri, na kujikita katika kuondoa daraja sifuri. Huo ni mkakati wa wilaya na ni mkakati wa serikali kupitia wizara ya Tamisemi kuhakikisha hakuna ufaulu wa daraja sifuri. Amesema ili kupigania mkakati huo lazima mwanafunzi atimize wajibu wake wa kusoma kwa bidii na kuzingatia masomo anayofundishwa darasani, na mwalimu amupe mwanafunzi mbinu na maarifa ya kujibu na kufaulu mtihani. Wakati huo huo mzazi atimize wajibu wa kumpatia mahitaji mwanafunzi na kusimamia vizuri katika malezi na ustawi wake wa kitaaluma.

Katika hatua nyingine Mh. Kayanda ametembelea zahanati ya Mang’ola Barazani ambayo wadau wa maendeleo shirika la world vision limeahidi kufanyia ukarabati jengo la mama na mtoto katika zahanati hiyo. Mh. Kayanda ametoa rai kwa mkandarasi kuanza kazi ya ukarabati mapema ili kuboresha miundo mbinu ya zahanati hiyo. Mh. Kayanda  amekagua hali ya upatikanaji wa dawa katika zahanati hiyo ya Mang’ola barazani na amehimiza wahudumu wa afya kubandika kwenye vituo vyao aina za dawa zinazopatikana ili wananchi waweze kufahamu. Amehimiza watendaji wa afya kufuata taratibu za kuweka na kutoa dawa kwa kuhakikisha  wanajaza kitabu cha rejesta ya dawa.

 



No comments:

Post a Comment

Punguza kilo tano kwa siku saba

  NI watu wachache wanaopenda kunenepa, wengi wanapenda miili ya wastani kwa kuwa  unene si mzuri. Ukiwa mnene si tu kwamba unakaribisha m...