Mamia ya waandamanaji walikusanyika katika mji mkuu wa Libya wa Tripoli, jana Ijumaa kupinga uamuzi wa wabunge wa kupitisha kura ya kutokuwa na imani na serikali ya mpito.
Hoja hiyo, iliyopitishwa Jumanne inawakilisha changamoto kwa mipango ya uchaguzi wa Desemba na inazuia juhudi za kuliunganisha taifa hilo lenye utajiri wa mafuta.
Serikali ya sasa ya mpito ya Libya ilichukua nafasi ya tawala mbili kinzani - moja iko mashariki mwa nchi na nyingine upande wa magharibi. Lengo kuu la serikali limekuwa ni kuandaa nchi kwa uchaguzi uliopangwa kufanyika Desemba 24.
Uchaguzi huo ulikuwa unatazamwa na wengi kama hatua kubwa ya kuelekea mwisho wa mgawanyiko mkubwa ambao umeshuhudiwa nchini humo.
Wakati huo huo, waziri mkuu Abdul Hamid Dbeibah ameapa kwamba serikali yake haitaondoka madarakani kabla ya kukabidhi madaraka kwa viongozi wapya.

No comments:
Post a Comment