Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia Wazee na Watoto, Dk Dorothy Gwajima amewaonya baadhi ya Waandishi wa habari wasio rasmi hasa wa mitandao ya kijamii wanaopotosha sanaa ya maneno anayotumia kwa lengo la kuongeza watazamaji kwenye mitandao yao waache kufanya hivyo.
Kauli hiyo ameitoa leo Alhamisi Agosti 19, 2021 mkoani Geita wakati akizungumza na kukabidhi vyerehani pamoja na viti mwendo vilivyotolewa na shirika lisilo la kiserikali la Plan International kwa wanafunzi waliokatisha masomo kwa kupata ujauzito na wanafunzi wenye ulemavu.
Waziri Gwajima amesema lengo lake lilikua kuondoa uvumi wa kuwa chanjo inaharibu nguvu za kiume.
"Mimi nilikua natumia sanaa ya maneno nikiwa na mkuu wa mkoa wa Mwanza, ili watu wasikie waelewe lakini wao wanatumia sanaa hiyo vibaya.
“Lengo letu ilikuwa kuondoa uvumi kuwa chanjo inaondoa nguvu za kiume nikamuuliza Mkuu wa Mkoa uko vizuri akasema idara yake iko vizuri na mimi nikamwambia hata wanawake waliochanja wako vizuri mitambo yao iko vizuri lakini waandishi feki wakabeba kwa lengo la kuharibu," amesema.
Amesema lengo lake ni kuonyesha jamii kuwa waliochanja hawajathirika, hivyo ni vema waandishi wakaacha kupotosha kwa lengo la kuongeza watazamaji na kuwataka kutomharibia kazi.
Amewataka waandishi kuelimisha jamii ili kuondoa uvumi unaorudisha nyuma juhudi za Serikali za kupambana na Uviko 19.
No comments:
Post a Comment