Iran imemuhukumu Nahid Taghavi mama Mjerumani mwenye asili ya Iran kifungo cha miaka 10 na miezi minane jela baada ya kutiwa hatiani kwa kuhusika na uendeshaji wa kundi lisilo halali na shughuli za propaganda dhidi ya utawala wa Tehran. Hayo yameripotiwa na shirika la habari la HRANA.
Nahid alitiwa mbaroni katika makazi yake mjini Tehran mnamo Oktoba 2020 baada ya kuwatembelea jamaa zake nchini Iran.
Amekuwa akizuiliwa katika gereza lenye ulinzi mkali la Evin mjini humo. Nahid alijulikana sana kama mwanaharakati wa haki za binadamu nchini Iran, hususan haki za wanawake na uhuru wa kujieleza.
Mama huyo mwenye umri wa miaka 67 aliishi mjini Cologne tangu 1983 na amekuwa na uraia wa Ujerumani tangu 2003.
Mtoto wake wa kike Mariam Claren amekuwa akihamasisha kuhusu kukamatwa mama yake tangu mwaka jana na amethibitisha hukumu iliyotolewa.

No comments:
Post a Comment