Rais wa Marekani, Joe Biden amesema operesheni ya kuwaondoa raia wa Marekani nchini Afghanistan pamoja na washirika wao wa Kiafghanistan, haitokwamishwa na magaidi. Matamshi hayo ameyatoa baada ya mashambulizi kutokea katika uwanja wa ndege wa Kabul na kusababisha mauaji ya takriban raia 60 wa Afghanistan na wanajeshi 13 wa Marekani.
Akizungumza jana usiku, Biden amesema Marekani itawasaka waliohusika na mashambulizi ya kujitoa muhanga ambayo kundi linalojiita Dola la Kiislamu, IS limekiri kuhusika.
Biden amesema hakuna ushahidi unaoonesha kuwa kundi la IS lilishirikiana na Taliban kufanya mashambulizi hayo ambayo yamewajeruhi watu wengine 140.
Aidha, Biden amethibitisha kwa mara nyingine tena kwamba Agosti 31 ndiyo siku ya mwisho ya majeshi ya Marekani kuondoka Afghanistan. Wakati huo huo, viongozi mbalimbali duniani wamelaani vikali mashambulizi hayo.

No comments:
Post a Comment