Tovuti ya habari ya Brazil ya UOL imeripoti kuwa Rais Jair Bolsonaro anadaiwa kuhusika katika kashfa ya kupunguza mishahara ya wasaidizi wake, madai hayo yakizidisha shinikizo zaidi kwa mwanasiasa huyo wa mrengo wa kulia.
Tovuti hiyo imenukuu kile ilichosema ni sauti za mkwewe wa zamani akielezea jukumu la Bolsonaro katika kashfa hiyo.Mpango huo wa utakatishaji fedha, unaojulikana kama rachadinha kwa lugha ya mtaani nchini Brazil, unahusisha kuajiri jamaa zako wa karibu kama wafanyikazi wa serikali na kisha kupokea kiasi fulani ya mishahara ya umma kutoka kwao.
Waendesha mashtaka mjini Rio de Janeiro wamefungua rasmi mashtaka dhidi ya seneta Flavio Bolsonaro, mtoto wa kwanza wa Rais Jair Bolsonaro, juu ya madai ya kushiriki kwake katika kashfa hiyo wakati alipokuwa mbunge.
Ufichuzi huu unatokea katika wakati ambapo Rais Bolsonaro aliyepata umaarufu wa kisiasa kwa kuahidi kupambana na ufisadi katika uchaguzi wa mwaka 2018, serikali yake inakabiliwa na madai ya ufisadi juu ya ununuzi wa chanjo ya Covaxin nchini humo.

No comments:
Post a Comment