Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Antonio Guterres ameliomba Baraza la Usalama la Umoja huo kuidhinisha nyongeza ya wanajeshi kwenye ujumbe wa kulinda amani nchini Mali, MINUSMA, kujibu kitisho kinachoongezeka cha mashambulizi ya makundi ya itikadi kali.
Guterres ametoa pendekezo hilo katika ripoti kwa wajumbe wa Baraza la Usalama ambayo hata hivyo bado haijawekwa hadharani lakini mashirika kadhaa ya habari yamefanikiwa kuiona.
Pendekezo hilo la kuongeza wanajeshi na polisi 2,069 kwenye ujumbe MINUSMA litafanya idadi jumla ya walinda amani kufikia 17,278 , idadi ambayo ni kubwa zaidi tangu ujumbe huo ulipoasisiwa mwaka 2013.
Kupitia ripoti hiyo, Guterres amesema nyongeza ya askari ni muhimu katika kukabiliana na uhalifu unaofanywa na makundi ya wanamgambo ambayo yanatanua operesheni zake kaskazini mwa Mali na kwenye mataifa jirani.

No comments:
Post a Comment