Kansela Angela Merkel wa Ujerumani amesema anaunga mkono wanajeshi wa nchi yake kuendelea kubakia nchini Mali licha ya kutokea mapinduzi ya kijeshi yaliyozusha mzozo wa kisiasa kwenye taifa hilo la Afrika Magharibi.
Merkel ametoa matamshi hayo baada ya kuzungumza na Rais Emmanuel Macron wa Ufaransa ambapo viongozi hao wawili wamekubaliana kuwa uwepo wa majeshi ya kigeni nchini Mali bado ni jambo muhimu.
Mamia ya wanajeshi wa Ujerumani wako nchini Mali chini ya ujumbe wa kulinda amani wa Umoja wa Mataifa, MINUSMA pamoja na mpango wa mafunzo ya kijeshi unaoratibiwa na Umoja wa Ulaya.
Ujerumani imesema licha wasiwasi uliopo kutokana na mapinduzi ya kijeshi yaliyotokea nchini Mali wiki iliyopita, bado ni jambo la busara kwa wanajeshi wa taifa kuendelea kusalia nchini Mali kutoa msaada kwa vikosi vya nchi hiyo katika kupambana na makundi ya itikadi kali.

No comments:
Post a Comment