Umoja wa Mataifa (UN) umetangaza kuwa dola bilioni 1 zinahitajika kupeleka misaada kwa Wasomali milioni 5.9 mwaka huu.
Katika taarifa iliyotolewa na Ofisi ya Uratibu wa Masuala ya Kibinadamu ya Umoja wa Mataifa (OCHA), ilielezwa kuwa watu milioni 2.7 nchini Somalia wapo kwenye hatari ya njaa kutokana na sababu kama vile mafuriko, uvamizi wa nzige, ukame na janga la corona.
Katika taarifa hiyo, ambayo iliripoti kuwa Wasomali milioni 2.6 walihama makazi yao kutokana na majanga ya asili na mizozo, ilielezwa kuwa jumla ya watu milioni 5.9 wanahitaji msaada wa kibinadamu mwaka huu.
Taarifa hiyo ilisema kwamba uhaba mkubwa wa maji unapatikana katika majimbo ya Somaliland, Puntland, Galmudug na Jubaland, na ilibainika kuwa takriban dola bilioni 1 zitaombwa kutoka kwa washirika wa kimataifa mwaka huu kwa ajili ya kusaidia.
UN na washirika wake walitumia dola milioni 820 katika kazi ya misaada ya kibinadamu nchini humo mwaka jana.
No comments:
Post a Comment