Mkuu wa Wilaya ya Moshi, Rajabu Kundya amesema wanachunguza chanzo cha moto ulioteketeza Mabweni manne ya Shule ya wasichana Sangiti iliyopo Kata ya Kirima Kibosho mkoani Kilimanjaro Tanzania.
Kundya ameyasema hayo leo Jumapili Februari 21,mwaka 2021 wakati alipofika Shuleni hapo kuangalia athari za moto huo ambapo umeunguza Mabweni hayo ambayo yalikuwa na jumla ya wanafunzi 180.
“Nimefika hapa leo kuwajulia hali kutokana na ajali ya moto mliyoipata, Serikali tunachunguza chanzo chake ambao umeteketeza Mabweni manne ili kubaini umesababishwa na nini,” amesema Kundya.
“Hii itasaidia kuwa sehemu ya mafunzo ya tahadhari ili majanga ya namna hii tuweze kuyadhibiti yasitokee, shule hii tunajua ina miundo mbinu mizuri ya moto kudhibiti moto, sasa nini kimesababisha, inabidi tuchunguze.”
Naye Mkuu wa shule hiyo, Sister Judita Massawe amesema moto huo ulitokea saa moja usiku na mpaka sasa chanzo chake huo hakijajulika.
“Moto ulianza saa moja usiku wanafunzi wakiwa madarasani, tulifanya juhudi za kuudhibiti kwa kushirikiana na majirani lakini mpaka sasa hatujajua chanzo chake, mabweni yaliyoungua ni ya wanafunzi wa kidato cha tatu na cha nne,” amesema Sisita Massawe

No comments:
Post a Comment