Rais wa Marekani Joe Biden amesaini maagizo matatu ya rais ya kuunganisha familia za wahamiaji zilizotenganishwa kutokana na sera ya utawala wa Trump na pia anataka kupitia tena ajenda yote ya uhamiaji kwa ukubwa zaidi.
Katika jaribio lake la kuzuia uhamiaji haramu, utawala wa Rais Donald Trump ulitenganisha watu wazima ambao hawakuwa na stakabadhi sahihi za uhamisho halali na watoto wao wakati wanavuka mpaka wa Marekani na Mexico.
Maagizo ya Bwana Biden yataanza kwa kuanzisha jopo kujaribu kuunganisha watoto wanaokadiriwa kuwa kati ya 600 na 700 ambao bado wametengana na familia zao.
Utawala wa Trump ulitenganisha watoto karibu 5,500 na wazazi wao ama waangalizi wao katika mpaka huo mwaka 2017-2018.
Utawala wa Rais Barack Obama - ambao Bwana Biden alikuwa makamu rais - pia ulitenganisha watoto na wazazi wao ambao hawakuwa na stakabadhi halali za kuishi Marekani, ingawa hilo lilikuwa nadra sana kutokea, kulingana na wanaharakati.
Moja ya maagizo ya Biden ni kuunda jopo litakaloongozwa na waziri mpya wa mambo ya ndani aliyeidhinishwa Alejandro Mayorkas - kufuatilia shughuli nzima ya watoto kuunganishwa tena na familia zao.
Maagizo ya pili na tatu ya Bwana Biden ambayo yaliwekwa saini Jumanne, yanaagiza kupitiwa tena kwa sera ya uhamiaji ya Bwana Trump ambayo ilikatisha utoaji wa hifadhi, ikapunguza shughuli za wahamiaji halali kuingia Marekani na kufuta ufadhili wa nchi za kigeni.
Akizungumza akiwa Ikuli, Bwana Biden amesema: "Tutafanyia kazi kufuta yaliyotekelezwa na utawala uliotangulia ambayo yanaenda kinyume na maadili na aibu kwa taifa, yaani kutenganisha watoto wakiwa mikononi mwa familia zao, mama na baba zao, mpakani bila mpangilio wowote wa kuunganisha watoto ambao bado wapo kizuizini na wazazi wao."
Bwana Biden pia amependekeza sheria ya kutoa hadhi ya makazi halali itakayotoa mwelekeo wa kupata makazi ya kudumu kwa raia wote takriban milioni 11 ambao hawana vyeti halali vya makazi.
Lakini wachanganuzi wanasema kuwa hadi kufikia sasa rais mpya amekwepa kubadilisha sera zenye msimamo mkali zilizotekelezwa na Trump ili kuzuia kuongezeka kwa uhamiaji haramu katika mpaka wa eneo la kusini.

No comments:
Post a Comment