Walinzi sita wameuawa baada ya kushambuliwa katika mbuga ya kitaifa ya Virunga mashariki mwa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo.
Maafisa wameelekezea kidole cha lawama kundi la waasi linalojulikana kama Mai-Mai, ambalo ni miongoni mwa makundi kadhaa ya waasi yanayohudumu katika eneo hilo.
Katika taarifa yake mbuga hiyo imesema uchunguzi wa awali unaashiria kuwa walinzi hao walivamiwa ghafla na hawakuwa na muda wa kujilinda na shambulio hilo lililotokea asubuhi Jumapili.
Ilisema mlinzi aliyejeruhiwa vibaya anapokea matibabu.
Walinzi hao walivamiwa walipokuwa wakifanya doria za kawaida ndani ya mbuga hiyo, kwa mujibu wa msemaji aliyezungumza na BBC.
Wafanyakazi katika mbuga hiyo ambayo huwahifadhi sokwe wa milimani wanaokabiliwa na tisho la kuangamia, wamekuwa wakishambuliwa mara kwa mara.
Mwezi Aprili mwaka jana walinzi 13 waliuawa na waasi baada ya kushambuliwa ghafla.

No comments:
Post a Comment