Timu ya kiongozi wa upinzani nchini Urusi Alexei Navalny imechapisha utafiti mpana kuhusu kasri la siri linalodaiwa kuwa lenye thamani ya mabilioni ya dola ambalo linamilikiwa na Rais wa Urusi Vladmir Putin.
Wanasema Putin alijenga jumba hilo la siri katika pwani ya Bahari Nyeusi, lenye thamani ya dola bilioni 1.33. Video ya saa mbili iliyowekwa kwenye YouTube inaelezea tuhuma za ubadhirifu wa fedha za umma na matumizi mabaya ya madaraka.
Ikulu imekanusha madai hayo huku msemaji wa Putin akisema rais hana kasri la aina hiyo. Filamu hiyo ilitengenezwa wakati Navalny alikuwa bado Ujerumani, ambako alikuwa akitibiwa kutokana na jaribio la mauaji kwa kupewa sumu inayoathiri mishipa ya fahamu mwezi Agosti.
Navalny, ambaye yuko kizuizini kwa sasa Urusi baada ya kukamatwa muda mfupi alipowasili Moscow Jumamosi, awali alitaka kuitoa mwenyewe ripoti ya utafiti huo baada ya kurudi nchini.

No comments:
Post a Comment