Nchi zinazojaribu kuyanusuru makubaliano ya nyuklia na Iran ya 2015 zimekubaliana kushughulikia uwezekano wa kuirudisha tena Marekani katika mpango huo chini ya utawala ujao wa Joe Biden.
Waziri wa Mambo ya Nje wa Ujerumani, Heiko Maas, ameionya Iran kutoipoteza fursa hiyo aliyoieleza kuwa ni ya mwisho.
Katika mkutano huo wa mtandaoni pamoja na mawaziri wenzake wa mambo ya nje, Maas amesema makubaliano hayo ya nyuklia yanazidi kupoteza muelekeo, kutokana na shinikizo la vikwazo vya Marekani dhidi ya Iran, pamoja na Iran kwa upande wake kukiuka masharti ya makubaliano hayo.
Marekani ilijitoa katika makubaliano hayo mnamo mwaka 2018, chini ya uongozi wa Rais Donald Trump.
Tangu wakati huo, nchi zilizobakia ambazo zimesaini mpango huo na Iran mwaka 2015 - Uingereza, Ujerumani, Ufaransa, China na Urusi - zimekuwa zikijaribu kuyanusuru makubaliano hayo.

No comments:
Post a Comment