Waziri Mkuu wa Ethiopia Abiy Ahmed amesema kuwa nchi yake iko tayari kupokea na kuwashika mkono maelfu ya watu wanatoroka makazi yao kwasababu ya mapigano yanayoendelea kaskazini mwa nchi hiyo eneo la Tigray.
Umoja wa Mataifa umesema kuwa karibu watu elfu 20 huenda wamevuka mpaka na kuingia nchi jirani ya Sudan katika kipindi cha siku 10 zilizopita.
Habari za hivi karibuni zasema jeshi la Ethiopia limechukua udhibiti wa eneo la kimkakati la Alamata.
Upande mwingine, chama cha Tigray People’s Liberation Front - TPLF kimeshtumu serikali kwa kufanya mashambulio ya anga katika mji wa Mekelle.
Hata hivyo imekuwa vigumu kuthibitisha madai yote hayo kwasababu umeme na mawasiliano yamekatwa katika eneo hilo.
Ethiopia imekataa wito wa kufanyika kwa mazungumzo na kusisitiza kuwa hatua hiyo itaendeleza uvunjaji wa sheria licha ya kuwa maelfu ya raia wanatorokea Sudan.
Waziri Mkuu Abiy ameahidi amani na kuunga mkono wale wanaorejea nchini humo lakini bado haifahamiki ikiwa hilo linaweza kufikiwa vipi wakati mapigano yanaendelea.

No comments:
Post a Comment