
SHIRIKISHO la Soka Tanzania (TFF) litapokea takribani kiasi cha fedha Dola 500,000 (Sh 1.1 bilioni) kutoka Shirikisho la Soka Duniani (FIFA) ili kusaidia uendeshaji wa shughuli za kimpira.
Fedha hizo ni sehemu ya mgawo wa takribani Dola 150 milioni (Sh 347 bilioni) ambao FIFA watautoa kwa nchi 211 ambazo ni wanachama wa shirikisho hilo.
Rais wa FIFA, Gianni Infantino amesema kuwa watahakikisha fedha hizo zinagawiwa haraka ili kusaidia wanachama wake kuendesha shughuli za kimpira wa miguu katika kipindi hiki ambacho idadi kubwa ya mashindano yamesimama kutokana na tatizo la kusambaa kwa virusi vya corona duniani.
"Ugonjwa huu umesababisha mabadiliko ambayo hayakutegemewa katika jumuiya ya mpira wa miguu na kama chombo kinachosimamia soka, ni jukumu la FIFA kuwa pamoja na kusapoti wale wenye mahitaji makubwa.
"Hii inaanzia kwa kutoa msaada wa haraka wa kifedha kwa vyama wanachama wetu ambao wengi wanakabiliwa na hali ngumu ya kiuchumi katika kipindi hiki," amesema Infantino.
Kwa mujibu wa Infantino, fedha hizo zitatolewa kabla ya kufika mwezi Julai ili zisaidie wanachama wake kujiendesha katika kipindi hiki cha janga la corona.
Pia mgawo huo utaenda sambamba na mgawo wa sehemu ya fedha iliyobakia kutoka katika mgawo wa shughuli za uendeshaji soka mwaka 2019 ambao haukuwa umekamilika.
No comments:
Post a Comment