Rais wa Tunisia Kais Saied ametangaza mipango ya kuifanyia marekebisho katiba na kuunda serikali mpya miezi kadhaa baada ya kumfuta kazi Waziri Mkuu na kusitisha shughuli za bunge, hatua ambayo wakosoaji wake wameiita mapinduzi.
Akizungumza na vituo viwili vya televisheni Jumamosi jioni, Saied amesema ataunda serikali mpya haraka iwezekanavyo atakapokamilisha kuchagua "watu wenye uadilifu mkubwa." Lakini hakutoa muda maalum wa kuunda serikali hiyo mpya.
Rais huyo wa Tunisia ameongeza kuwa ni muhimu kuibadilisha katiba. Hatua yake imekosolewa vikali na majaji na wapinzani, hasa chama cha kiislamu cha Ennahdha chenye viti vingi bungeni.
Nchi hiyo iliyosifiwa kwa kuwa na demokrasia imara katika kanda ya mataifa ya kiarabu, imetumbukia kwenye mzozo wa kisiasa na wa kiuchumi pamoja na kuathirika na janga la Covid-19.

No comments:
Post a Comment