Mawaziri na makatibu wakuu wote wa Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania (SMT) na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar (SMZ) leo wanaanza vikao vya ndani kujadili kero za Muungano.
Tangu kuanzishwa utaratibu wa kushughulikia hoja za Muungano kupitia vikao vya kamati ya pamoja ya SMT na SMZ mwaka 2006, hoja 25 zimejadiliwa na mpaka sasa hoja saba zimepatiwa ufumbuzi huku hoja 18 zikiendelea kutafutiwa ufumbuzi.
Alizungumza na vyombo vya habari Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais, Muungano na Mazingira, Seleman Jafo amesema lengo la vikao hivyo vinavyoanza leo Agosti 23, 2021 ni kuimarisha Muungano.
"Makatibu wakuu na mawaziri wote SMT na SMZ tupo hapa Zanzibar kwa ajili ya vikao hivi muhimu kwa mustakabali wa Muungano wetu vitakavyofanyika Agosti 23 na 24, 2021," amesema.
Amesema baada ya kikao cha mawaziri wajumbe watapata fursa ya kutembelea miradi ya kimkakati ya Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Abeid Aman Karume (Terminal III) na Kiwanda Cha maziwa Cha Bakhresa ambayo ni miongoni mwa hoja za Muungano ambazo zimekuwa zikitafutiwa ufumbuzi.
Hoja tano ambazo zimepatiwa ufumbuzi ni pamoja na utekelezaji wa sheria ya haki za binadamu Zanzibar na utekelezaji wa sheria ya haki za usafiri majini.
Zingine ni ushirikishwaji wa SMZ kwenye masuala ya kimataifa na kikanda, ushiriki wa Zanzibar katika Jumuiya ya Afrika Mashariki utafutaji na uchimbaji mafuta na gesi asilia.
Nyingine ni gharama za kushusha mizigo Bandari ya Dar es Salaam kwa mizigo inayotoka Zanzibar na utaratibu wa vikao vya kamati ya pamoja ya SMT na SMZ.
Kaimu Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais Sera, Uratibu na Baraza la Wawakilishi, Dk Saada Mkuya amesema baada ya majadiliano ndipo watasema ni hoja gani zitakuwa zimepatiwa ufumbuzi na kusainiwa hati ya kuziondosha.
"Huu ni utaratibu wa kawaida, unajua mnapokuwa pamoja hamuwezi kwenda kwa asilimia 100, ndio maendeleo," amesema.

No comments:
Post a Comment