Tanzania imeshika nafasi ya saba kati ya nchi 10 bora ndani ya Bara la Afrika zinazotangaza vyema vivutio vyake vya utalii, ripoti hiyo imetolewa kwenye mkutano wa Kimataifa wa utalii wa kanda ya Afrika ulioandaliwa na Shirika la Kimataifa la Utalii Duniani (UNWTO).
Ripoti hiyo imetolewa nchini Namibia mapema leo ambapo pia Tanzania imetajwa kuendelea kuongoza na kufanya vizuri katika sekta ya utalii licha ya uwepo wa changamoto wa ugonjwa wa COVID-19 ambao umeyakumba karibu Mataifa mbalimbali Duniani kote.
Katika mkutano huo, Waziri wa Maliasili na Utalii, Dkt. Damas Ndumbaro, akiwa ameambatana na Watalaamu wake kutoka Wizara ya Maliasili na Utalii walishiriki ambapo Dkt. Ndumbaro, amesema Tanzania imejaliwa kuwa na vivutio vingi na vya kipekee ambavyo havipatikani mahali popote Duniani isipokuwa Tanzania.
Tanzania inaingia kwenye 10 bora kwa mara ya tatu mfululizo na imekuwa na vivutio mbalimbali vinavyotamba Duniani ikiwemo mlima mrefu barani Afrika, Mlima Kilimanjaro, Hifadhi ya Serengeti, Hifadhi ya Nyerere, Hifadhi ya Ruaha, Tarangile pamoja na Mamlaka ya Hifadhi ya Eneo la Ngorongoro.

No comments:
Post a Comment