Umoja wa Mataifa umesema zaidi ya walinda amani 100 wa zamani kutoka Ethiopia wametafuta ulinzi wa kimataifa na wameomba hifadhi nchini Sudan.
Walikuwa sehemu ya ujumbe wa UN uliofungwa hivi karibuni huko Darfur.
Hii inakuja baada ya walinda amani wengine wa Ethiopia awali kutoka eneo la mzozo la Tigray - kukataa kurudi Ethiopia kwa kuhofia kuteswa.
Kuna wasiwasi unaoongezeka juu ya madai ya ukatili uliofanywa wakati wa mzozo wa miezi sita huko Tigray.
Umoja wa mataifa umesema badala ya kurudi nyumbani wakati operesheni ya ujumbe wao ilipomalizika katika mkoa wa Darfur, karibu walinda amani 120 wa Ethiopia waliomba hifadhi nchini Sudan.
Maendeleo haya yanaweza kuhusishwa na mivutano ya kikabila ambayo imezidi nchini Ethiopia kutokana na mzozo katika eneo la kaskazini mwa Tigray.
Mwezi Februari huko Sudan Kusini kundi jingine la walinda amani wa Ethiopia ambao walikuwa asili ya Tigray walikataa kwenda nyumbani wakisema wanahofia kuteswa.
Kumekuwa na ripoti nyingi za ukiukwaji wa haki za binadamu wakati wa mzozo wa miezi sita. Jumamosi mkuu wa Kanisa la madhehebu ya Orthodox la Ethiopia - yeye mwenyewe wa kabila la Tigray - alisema ukatili huo ni mauaji ya kimbari.

No comments:
Post a Comment