Mkuu wa Mkoa wa Dodoma Dkt Binilith Mahenge amemuagiza Mkuu wa Wilaya ya Dodoma Josephat Maganga kukaa na kuzungumza na Mkuu wa polisi Wilaya ya Dodoma (OCD) kwa lengo la kudhibiti askari polisi wanaokuwa doria nyakati za usiku kutengeneza mazingira ya kupata rushwa katika maeneo ya biashara za vileo nyakati za usiku.
Dkt Mahenge amefikia uamuzi huo baada ya kukutana na wafanya biashara wa vileo ofisini kwake kwa lengo la kusikiliza kero zao, ambapo wamemueleza kuwa pindi wakizidisha mda wa kufunga maeneo yao ya biashara wamekuwa wakisumbuliwa na askari wanaokuwa doria wakitaka rushwa.
“Hili sijasikia hapa tu hata huko mitaani nimesikia mara nyingi kwamba kuna vikosi ukizindisha mda kidogo wanafika na kutengeneza mazingira ya kupokea rushwa, nikutake mheshimiwa DC (Mkuu wa Wilaya) kakae na OCD hili sasa limekuwa kero, na mimi nitaongea na RPC sitaki tena kusikia hili” amesema Dkt Mahenge.
Amemtaka OCD Wilaya ya Dodoma kuwakemea askari wote wanaokuwa doria nyakati za usiku wenye tabia ya kuomba rushwa toka kwa wafanyabiashara na kuwataka waache mara moja kwani vitendo hivyo vinaliletea sifa mbaya jeshi la polisi.
Kwa upande mwingine amewataka wafanyabiashara kufuata mashaeti ya leseni zao na kuepuka kutoa rushwa pindi wanapofanya makosa badala yake watoe taarifa aidha walipe faini au kufanya maongezi na mamlaka husika na sio kutoa rushwa.
Ameongeza kuwa “na ninyi sasa mfuate masharti ya leseni zenu kuepuka haya mambo, ukiambiwa funga bar saa tano au saa sita funga, umepewa leseni ya glocary hakikisha una mfungia mteja anakwenda kunywea nyumbani, kama unataka uhudumie hapo tafuta leseni ya bar” amesema.
Amesema wamekutana na kundi hilo kwa kuwa wanatamani kuona jiji la Dodoma linakuwa la kisasa kwa kuwa na huduma mbalimbali na nzuri ambazo zitawavutia wateja, sambamba na kuwa eneo salama kwa wananchi na mali zao wanapotafuta mahitaji yao muhimu wale salama bila kusumbuliwa na kitu chochote.
“Hapa tunapokea wageni mbalimbali kutoka nchi tofauti tofauti tunataka wakija hapa wahudumiwe vizuri kama ni hoteli na bar ahudumiwe vizuri ili hata akirudi kwao apakumbuke Dodoma, lakini sio amekuja hapa usiku kapumzika anapigiwa kelele za mziki usiku mzima hii sio sawa kabisa tunataka wawe salama” amesema.
Aidha ameitaka halmashauri ya jiji la Dodoma na balaza la taifa hifadhi na usimamizi wa mazingira NEMC kuandaa vipeperushi vyenye masharti yote na maonyo yanayohusu biashara ya vileo na kuvibandika kila eneo lenye biashara hiyo kusaidia kuwakumbusha wamiliki wa maeneo hayo ya biashara.
Kwa upande wake Mkurugenzi wa Jiji la Dodoma bw. Joseph Mafuru amesema jiji wameandaa mpango kabambe wa ardhi wa miaka 20 katika eneo lote la jiji ili kusaidia kuepusha migongano ya matumizi ya ardhi kwa kupanga kila eneo na matumizi yake kama makazi, biashara, viwanda na taasisi mbalimbali.
Amesema katika eneo la biashara ya vileo ni muhimu sana kwa jamii inayotumia vileo lakini wamiliki wake wamekuwa wakikiuka masharti ya leseni zao kwa kuongeza biashara nje ya makubaliano au nje ya leseni yake ambapo wanaomba leseni ya glocary lakini akikaguliwa anakubwa akiuza kama bar.
Aidha kuhusu baadhi ya bar kukesha na kupiga mziki usiku kucha amesema wale wanaohitaji kukesha lazima waombe leseni ya night clabu ambayo pia ina masharti yake yanayotakiwa kufuatwa ili kutokuwasumbua watu wengine.
Nae Meneja wa baraza la taifa la hifadhi na usimamizi wa mazingira NEMC kanda ya kati Frankline Rwezimula, amesema kunasheria inayosimamia uchafuzi wa mazingira kwa njia ya sauti ambayo inafanya kazi katika viwanda, mitambo, magari na sehemu za starehe kama bar na kila sehemu inakuwa na kiwango chake cha sauti kwa majira ya mchana na usiku.
Amesema mara kwa mara wamekuwa wakipokea malalamiko kutoka kwa wananchi wanaoishi maeneo jirani na sehemu za starehe kuwa wamekuwa wakipiga mziki kwa sauti ya juu jambo ambalo ni kinyume na sheria ambapo unaweza kupigwa faini.
Baadhi ya wafanyabiashara waliopata nafasi ya kuongea wameahidi kufuata sheria pia wametoa kero mbalimbali ikiwamo kuiomba serikali kuwaongezea muda wa kufungua biashara zao kutoka muda wa sasa wa saa kumi jioni ambapo biashara zao zimekuwa hazifanyi vizuri wakati tozo na kodi zikiwa vilevile na kuwapa wakati mgumu.

No comments:
Post a Comment