Mkuu ajaye wa shirika la biashara ulimwenguni, WTO Ngozi Okonjo-Iweala ameonya dhidi ya kukosekana kwa mshikamano wa kimataifa katika mgawanyo wa chanjo dhidi ya virusi vya corona, akisema hali hiyo inaweza kupunguza kasi ya kukabiliana na janga la COVID-19 na kudhoofisha ukuaji wa uchumi kwa mataifa masikini na hata matajiri.
Dr. Ngozi ameliambia shirika la habari la Reuters kwamba kipaumbele chake cha juu kilikuwa ni kuhakikisha WTO inafanya zaidi katika kuushughulikia mzozo huo, akisema wanachama wanatakiwa kuharakisha kuondoa vizuizi vya kuuza nje vinavyodhoofisha biashara ya dawa na vifaa vinavyohitajika.
Dr. Ngozi, waziri wa zamani wa fedha wa Nigeria aliteuliwa jana Jumatatu na anatarajiwa kuanza rasmi majukumu yake Machi Mosi.
Ni mwanamke na mwafrika wa kwanza kuongoza chombo hicho chenye wanachama 164.
Pamoja na mwito huo, amesema suala atakalolipatia kipaumbele atakapoanza majukumu yake ni hatua za kukabiliana na anguko la kiuchumi lililosababishwa na COVID-19.

No comments:
Post a Comment