Rais wa Nigeria Muhammadu Buhari ameidhinisha pesa kiasi cha dola milioni 17 kwa ajili ya kuanzisha vituo vya utoaji oksijeni katika maeneo 38 kote nchini humo lengo likiwa ni kuimarisha matibabu ya ugonjwa wa virusi vya corona kwa wanaotaka oksijeni.
Katika taarifa, serikali imesema imetenga dola 671,000 kwa uboreshaji wa vifaa vya utoaji wa oksijeni vilivyopo katika hospitali tano wakati nchi hiyo inakabiliana na tatizo la ukosefu wa oksijeni kwasababu ya wimbi la pili la virusi vya corona.
Bado haijafahamika ni lini mradi huo wa oksijeni utakamilika.
Lakini waziri wa fedha Zainab Ahmed ametoa taarifa katika mkutano wa Baraza la Taifa la Kiuchumi uliohudhuriwa na magavana wa majimbo na naibu rais Yemi Osinbajo kuwa hatua ya kutoa fedha hizo kumetokana na kuongezeka kwa idadi ya wagonjwa wanaohitaji oksijeni kwasababu ya kuongezeka kwa maambukizi ya virusi vya corona nchini humo.
Alhmisi, Nigeria ilirekodi idadi ya maambukizi 1964 ikiwa ndio idadi ya juu zaidi kwa siku hadi kufikia sasa.
Kwa mujibu wa taarifa kutoka kituo cha udhibiti wa magonjwa Nigeria,nchi hiyo imerekodi jumla ya maambukizi 116,655 ya virusi vya corona ikiwemo 93, 000 walipona na vifo 1485 vilivyothibitishwa.
Bado haijulikani ni wagonjwa wangapi wanaohitaji usaidizi wa kupumua kwa kutumia oksijeni nchini humo lakini mamlaka inasema kuwa hali ni tete.

No comments:
Post a Comment