Search This Blog

Thursday, December 31, 2020

Wakulima kutoka wilaya 25 wapatiwa mbegu


Na John Walter ,Arusha.

Wakulima kutoka Wilaya 25 zilizoko nchini wamepatiwa msaada wa mbegu tani 200 kutoka kampuni ya Bayer  zitakazowasaidia kuongeza uzalishaji na kukuza vipato vyao .

Akizungumza katika uzinduzi wa Mpango  wa  “Mashamba Bora ,Maisha Bora”  uliofanyika jijini Arusha ,Meneja wa Kampuni ya Bayer Nchini Tanzania, Frank Wenga alisema kuwa kwa kushirikiana na Tume ya Kilimo Tanzania (ACT) watasambaza takribani tani 200 kwa Wilaya 25 zilizoko nchini Tanzania mchango ambao una thamani ya shilingi bilioni 1.1

Meneja huyo amesema kuwa mpango huo umeshazinduliwa katika nchi za Kenya,Nigeria,Zambia,Malawi,Afrika Kusini na Msumbiji ambapo wakulima wadogo 700,000 barani Afrika watanufaika kati ya mwaka 2020 hadi 2022 huku nchini Tanzania Wakulima 100,000 watanufaika.

Akizindua Mpango huo na kukabidhi mbegu kwa wakulima wa Wilaya ya Meru ,Mkurugenzi Mtendaji wa Chama cha Wafanyabiashara wa Mbegu Tanzania (TASTA) ,Bob Shuma amewataka Wakulima waliopokea mbegu hizo kuzitumia vizuri kwa kushirikiana na wataalamu wa kilimo ili waweze kupata mavuno mengi na kuwa mfano wa kuigwa kwa wengine.

“Tunashukuru serikali kwa kuweka miundombinu bora katika kilimo na vituo vya masoko ya mazao ili kuwasaidia wakulima ,kwa kushirikiana na sekta binafsi tunaweza kuinua kilimo na kuleta mabadiliko chanya” Alisema Bob

Mwakilishi wa Ofisi ya Kilimo Mkoa wa Arusha , Chisunga Jumanne amepongeza juhudi za kampuni ya Bayer katika kuwakumbuka wakulima na kuwarudishia sehemu ya faida wanayoipata kwa kuwapa msaada wa mbegu jambo ambalo linapaswa kuigwa na makampuni mengine.

Kwa upande wao Wakulima walipokea Mbegu hizo kutoka Wilaya ya Meru  Ndetaiyo Nko na Anna Mbaga wameishukuru kampuni ya Bayer na kuahidi kutumia mbegu hizo kusaidia kuongeza uzalishaji katika kilimo hivyo kukuza vipato vyao.



No comments:

Post a Comment

Punguza kilo tano kwa siku saba

  NI watu wachache wanaopenda kunenepa, wengi wanapenda miili ya wastani kwa kuwa  unene si mzuri. Ukiwa mnene si tu kwamba unakaribisha m...