NA ANDREW CHALE, CHALINZE
HALMASHAURI ya Chalinze, Mkoani Pwani imetekeleza maagizo ya Waziri Mkuu Kassim Majaliwa kwa kutengeza madawati 355, meza na viti 221, huku Mbunge wa Jimbo hilo Ridhiwani Kikwete akichangia shilingi milioni 3.67 kuunga mkono zoezi hilo.
Akizungumza wakati wa kupokea madawati hayo zoezi lilofanyika Mioni Wilayani Bagamoyo, Mbunge wa Chalinze, Ridhiwani Kikwete amesema kuwa madawati hayo ni kwaajili ya shule 38, ambapo za Sekondari 20 na shule za msingi 18.
Kikwete amesema kuwa lengo ni kuhakikisha hakuna mwananfunzi anayekaa chini
"Lengo letu ni kuona wanafunzi wote wanakaa kwenye madawati ili waweze kuandika vizuri wanapokuwa darasani na kuacha kukaa chini darasani” Amesema Kikwete
Madawati hayo yamepokelewa mbele ya Mkuu wa Mkoa wa Pwani Evarist Ndikilo na Mkuu wa Wilaya ya Bagamoyo Bi Zainab Kawawa.
Awali wakati wa kupokea madawati hayo, Mkuu wa Mkoa wa Pwani, Evarist Ndikilo aliipongeza Halmashauri ya Chalinze kwa kuvuka lengo la uhaba wa madawati.
"Niwapongeze sana kwa kutimiza lengo la madawati mashuleni. Kwa maana urithi mkubwa kwa watoto wetu ni elimu. Elimu ni msingi bora, elimu ndio kila kitu, elimu ndio urithi.
Mkoa wetu wa Pwani kielimu tunahitaji kuwa nafasi ya kwanza pale juu ama tatu bora kwa maana mwaka 2018 Pwani tulishika nafasi ya 11 kati ya 26, 2019 tulipata nafasi ya 10 na mwaka huu 2020 tumeweza kuwa nafasi ya 9, lengo tufikie pale juu." Alisema Ndikilo
Aidha, Ndikilopia aliweza kukabidhi madawati hayo na meza na viti kwa wawakilishi wa shule mbalimbali waliofika katika tukio hilo lililofanyika katika viwanja vya shule ya Kikalo, Miono.




No comments:
Post a Comment