Na Ezekiel Mtonyole – Dodoma.
Serikali ya Tanzania kwa kushirikiana na Chuo cha ufundi stadi cha Henan cha nchini China wanatarajia kuanza kujenga chuo cha ufundi stadi kitakachokuwa kikizalisha wataalamu wa Kilimo na Ufugaji Wilayani Kongwa Mkoani Dodoma.
Hayo yamebainishwa Wilayani Kongwa Mkoani Dodoma na Waziri wa Elimu Sayansi na Teknolojia Profesa Joyce Ndalichako wakati wa ziara yake ya kukagua miondombinu ya elimu katika Wilaya hiyo ambapo amesema chuo hicho ni kupanua wigo wa wataalamu hapa nchini.
“Tupo katika mchakato wa kujenga chuo hicho tukishirikiana na wenzetu wa chuo cha Henan China tunasubiri tu mchakato wa fedha ili chuo kianze kujengwa hapa Kongwa” amesema Waziri Ndalichako.
Amesema Chuo hicho cha China kimeonesha kinalengo la kushirikiana na Tanzania katika kuinua sekta ya kilimo na mifugo hapa nchini wakishirikiana na Mamlaka ya elimu ya mafunzo na ufundi stadi VETA kutoa mafunzo hayo.
Wakati huo huo Waziri Profesa Ndalichako amebainisha kuwa katika kukabiliana na tatizo la uhaba wa vyumba vya madarasa Serikali kupitia mradi wa kuimarisha shule za Sekondari wamepanga kujenga shule elfu moja (1000) katika maeneo mbalimbali hapa nchini.
Amesema mara kwa mara katika kipindi kama hiki Serikali huwa bize kukabiliana na uhaba wa vyumba vya madarasa lakini kuanzia mwakani watajenga idadi hiyo ya shule za Sekondari kuepusha ushumbufu huo ambao hutokea mara kwa mara katika kipindi hiki.
“Kila mwaka katika kipindi kama hiki tunakimbizana mpaka tunazuia likizo kwa Wakurugenzi wa Halmashauri yote ni kuhakikisha watoto wanaingia madarasani hii tunataka tuikomeshe kabisa” Amesema Prof. Ndalichako.
Pia ameiagiza Mamlaka ya Elimu Tanzania TEA kwenda kumalizia mradi wa ujenzi wa Hosteli za wasichana katika shule ya Sekondari Kibaigwa mradi ambao waliuanza bila kuumalizia wakati wa kipindi cha uongozi wa nyuma wa mamlaka hiyo.
Aidha amesema Serikali itafanya kila jitihada ili kuboresha miondombinu ya elimu katika Wilaya ya Kongwa sambamba na ujenzi wa shule mpya eneo la Kibaigwa ili kuepusha msongamano katika wa wanafunzi katika shule hiyo.
Kwa upande wake Mkurugenzi Mkuu wa VETA Dkt Pancras Bujulu akifafanua kuhusu mradi wa ujenzi wa Chuo cha VETA kipya amesema andiko la mradi limekamilika na wana subiri taratibu za ujenzi zitaanza mapema baada ya kukamilika kwa taratibu za serikali.
Nae Mbunge wa jimbo la Kongwa ambaye pia ni Spika wa Bunge Mhe. Job Ndugai ameshukuru serikali kwa kujenga vyuo vya VETA katika Wilaya hiyo kwani kwa mda mrefu Wilaya ya Kongwa iliachwa nyuma katika miradi kama hiyo na kubainisha kuwa wananchi wanafuraha sana ujio wa Chuo cha VETA ambacho kipo mbioni kukamilika.
Amesema kuna vijana wengi wanamaliza kidato cha nne katika Wilaya hiyo lakini walikuwa hawana pa kwenda lakini ujio wa vyuo hivyo utasaidia kutafuta ujuzi katika vyuo hivyo vinavyojengwa na Serikali.
Katika ziara hiyo Waziri Profesa Ndalichako amekagua ujenzi wa ofisi za mdhibiti ubora wa elimu Wilaya ya Kongwa, ujenzi wa chuo cha ufundi stadi VETA, Shule ya Sekondari Ibwaga na Shule ya Sekondari Kibaigwa.
No comments:
Post a Comment