Wajasiliamali wadogo jijini Mwanza wamesema wanasubiri kwa hamu ujio wa mgombea urais Kupitia Chama cha Mapinduzi (CCM), DK.John Magufuli ili wasikie sera zake kwani Kwa kipindi cha miaka mitano pekee amekuwa msaada mkubwa kwao hasa kwa kuleta vitambulisho vya mjasiliamali.
Wakizungumuza kwa nyakati tofauti wafanyabiashara hao maarufu kama machinga walisema toka Dk.Magufuli amekuwa rais amewafanya wajasiliamali wengi kufanya kazi yao pasipo kubughudhiwa na kujiona nao wana nafasi kwenye nchi yao.
Magdalene Mbuto mfanyabiashara wa viungo vya chakula katika mtaa wa liberty jijini hapa alisema anamusubiri kwa hamu Rais Magufuli na ataendelea kumushukuru daima baada ya kuleta vitambulisho vya mjasiliamali kwani amewafanya waendeshe biashara zao bila kero yeyote
Alisema awali kabla ya kupewa vitambulisho vya mjasiliamali walionekana kama wafanyabiashara haramu lakini kwa sasa wanaendesh shughuli zao bila kusumbuliwa na imewasaidia kujikwamua kiuchumi siku hadi siku.
John Malongo ambaye ni machinga katika soko maarufu la wafanyabiashara wadogo Makoroboi alisema toka amepokea kitambulisho cha mjasiliamali amekuwa na amani na kazi anayoifanya kwani anajiona kazi yake imerasiishwa.
Malongo alisema inafikia hatua anapovaa kitambulishi hicho anajiona kama mfanyakazi wa umma kwa kuwa anajiamini na kufanya kazi bila wasiwasi na hivyo ataendelea kumuunga mkono Dk.Magufuli hata atakapoondoka madarakani.
Alisema hadi sasa anasubiri kwa hamu kampeni za Dk. Magufuli jijini Mwanza kwani anaamini ana sera zenye tija ambazo huenda zikaongeza neema kwa wananchi wa kawaida ikiwemo wafanyabiashara wadogo.
Juliyana Mapegere maarufu kama "Bibi Mkubwa" ambaye ni muuza karanga katika barabara ya Kenyata alisema watanzania wana bahati sana kupata kiongozi anayejali shida za wanyonge ambapo alisisitiza kuwa ingawa umri wake umeenda (miaka 65) lakini hadi sasa ameshanufaika na uwepo wa magufuli na kusisitiza kuwa atafanya kila liwezekanalo kwenda kusikiliza kampeni za mgombea huyo.
Ikumbukwe kuwa Dk Magufuli anatarajiwa kuwasili jijini Mwanza siku ya jumapili ambapo atapita wilayani Magu kuzungumuza na wananchi na siku inayofuata atafanya mkutano wa kampeni kunadi sera za CCM katika uwanja wa CCM-Kirumba.

No comments:
Post a Comment