Search This Blog

Sunday, March 8, 2020

Mbunge Azza akabizi taulo za kike zenye thamani ya shilingi milioni 7.7

Mbunge wa Viti Maalumu Mkoa wa Shinyanga Mhe. Azza Hilal Hamad (CCM) amekabidhi Taulo laini za kike ‘Pedi’ zinazofuliwa zenye thamani ya shilingi milioni 7.7 zilizotokana na mchango wake kwa kushirikiana na wadau mbalimbali wa maendeleo mkoani Shinyanga kwa ajili ya wanafunzi 780 wanaotarajia kuhitimu elimu ya darasa la saba mwaka 2020 kutoka shule 30 mkoa wa Shinyanga.

Mhe. Azza amekabidhi taulo hizo leo Jumapili Machi 8,2020 wakati wa Maadhimisho ya siku ya wanawake Duniani ambapo katika mkoa wa Shinyanga yamefanyika katika kijiji cha Iselamagazi kata ya Iselamagazi halmashauri ya wilaya ya Shinyanga.

Mhe. Azza ambaye ndiye alikuwa mgeni rasmi, amesema taulo hizo laini zinazofuliwa ni kwa ajili ya kuwaandaa wanafunzi wa kike wanaotarajia kumaliza elimu ya darasa la saba mwaka 2020.
“Takwimu zinaonesha kuwa watoto wengi wa kike wanapokuwa katika siku zao ‘Hedhi’ huwa hawaendi shuleni kutokana na mazingira wanakotoka hivyo kupoteza masomo yao. Kutokana na hali hii nilikaa nikafikiria namna ya kuwasaidia watoto wetu,nikashirikisha wadau mbalimbali ambao waliniunga mkono,tukaanza kuchangishana na kufanikiwa kupata shilingi Milioni 7, laki 7 na 78 elfu kwa ajili ya taulo laini”,amesema Azza.

“Nimefanikiwa kupata maboksi 66 yenye pakti 12 ambapo ndani ya kila pakti kuna taulo nne. Taulo hizi tunazigawa katika halmashauri zote 6 za wilaya mkoa wa Shinyanga,kila halmashauri itapata taulo laini 130.Tutawapatia wanafunzi 780 kutoka shule 30 ambapo tutatoa kwa shule 5 zilizopo pembezoni kwa kila halmashauri”,ameeleza Mhe. Azza.
Mbunge huyo alisema kila mwanafunzi atapatiwa pakti moja ambayo ina taulo laini za kike nne ambazo atazitumia kwa kipindi cha mwaka mzima kwani kila taulo laini inatumika kwa muda wa miezi mitatu.

“Naomba Wakurugenzi wa halmashauri mhakikishe mnagawa hizi taulo laini kwa watoto wa kike wanaotoka katika mazingira magumu.Tunataka watoto wa kike wakae darasani muda wote ili waweze kufanya mtihani wa kumaliza darasa la saba vizuri”,ameongeza Azza.
Mhe. Azza ametumia fursa hiyo kuwapongeza wadau mbalimbali waliojitokeza kumuunga mkono kufanikisha Kampeni yake ya kumuandaa msichana kufanya mtihani wa darasa la saba 2020 kwa kumpatia Taulo za kike.

“Miongoni mwa wadau walioniunga mkono ni serikali ya mkoa wa Shinyanga,Shirika la VSO, Agape,Life Water International,Benki ya CRDB na Kampuni ya Vinywaji Baridi ya Jambo Food Products Ltd pamoja na marafiki zangu ,viongozi,wananchi na wadau wa maendeleo mbalimbali wa maendeleo” ,amefafanua Mhe. Azza.

Afisa Maendeleo ya Jamii Mkoa wa Shinyanga Tedson Ngwale amesema taulo  laini za kike zinamfanya mtoto wa kike kujiamini na kuhudhuria masomo yake bila kikwazo hivyo inaongeza nafasi ya watoto kufanya vizuri katika masomo yao.
Aidha amewaomba wadau wasaidie kutoa elimu ya matumizi sahihi ya pedi kwa watoto wa kike ikiwemo kuwashauri kutozianika uvunguni bali sehemu yenye jua na mwanga wa kutosha na wazifue pedi hizo kwa maji moto.
ANGALIA PICHA HAPA CHINI

No comments:

Post a Comment

Punguza kilo tano kwa siku saba

  NI watu wachache wanaopenda kunenepa, wengi wanapenda miili ya wastani kwa kuwa  unene si mzuri. Ukiwa mnene si tu kwamba unakaribisha m...