
LONDON, ENGLAND . STRAIKA, Harry Kane sasa anashika namba sita kwa wakali wa mabao wa muda wote wa timu ya taifa ya England, akiwapiku Alan Shearer, Nat Lofthouse na Tom Finney baada ya kufanya maajabu yake katika mechi ya 1,000 ya kikosi hicho cha Three Lions.
Kane, anayekipiga kwenye kikosi cha Tottenham Hotspur alipiga hat trick matata, ambapo lilikuwa bao lake la 29, 30 na 31 kwa England na kuisaidia timu hiyo kuongoza mabao 5-0 dhidi ya Montenegro hadi mapumziko. Mechi hiyo ilimalizika kwa England kushinda 7-0 na hivyo kufuzu mikikimikiki ya Euro 2020.
Kwa kufunga hat-trick kwenye mechi hiyo, Kane sasa amewapiku magwiji watatu wa timu hiyo, lakini sasa akiwa amezidiwa mabao tisa tu na Michael Owen, anayeshika nafasi ya tano. Wayne Rooney ndiye anayeshikilia rekodi ya mabao kwenye kikosi hicho cha England, mabao 53.
Kutokana na hilo, Kane anahitaji mabao 22 kuweza kufikia rekodi hiyo ya Rooney, huku wengi wakimpa nafasi ya kwenda kuifikia rekodi hiyo na kuivunja kutokana na uhodari wake wa kufunga na umri alionao kwa sasa.
No comments:
Post a Comment