Na John Walter-Manyara
Wajumbe wa Mkutano Mkuu wa Shirikisho la Riadha mkoa wa Manyara, wamempigia kura za kishindo Safari Ingi kuendelea kuwa Mwenyekiti wa Shirikisho hilo katika kipindi kingine.
Ingi ambaye amegombea kwa Mara ya pili nafasi hiyo, alishinda kwa kura zote za wajumbe 8 waliopiga kura.
Akitangaza matokeo ya uchaguzi huo uliofanyika Desemba 23,2020 katika ukumbi wa mikutano ofisi ya mkuu wa mkoa wa Manyara, Mwenyekiti wa Kamati ya Uchaguzi Charles Maguzu aliwataja viongozi hao na kura walizopata.
Nafasi ya Makamu Mwenyekiti ilichukuliwa na Wema Dosla bila mpinzani kwa kura 8.
Kwenye nafasi ya Katibu iliyokuwa ikishindaniwa na watu wawili, Pascal Athanas Mwalimu wa shule ya msingi, pia anayo stashahada ya Michezo na uongozi, mwalimu wa Michezo na ana kibali cha kuchezesha ligi kuu Tanzania alipata kura 2 akishindwa na Gwatema Simon aliepata kura 6.
Msimamizi wa uchaguzi alimtangaza Gidamis Shahanga kuwa mjumbe wa mkutano mkuu taifa baada ya kupata kura 8 nafasi ambayo hakuwa na mpinzani.
Nafasi ya Wajumbe wa kamati tendaji imechukuliwa na Andrea Mao aliepata kura 7, Mwalimu Sabina Karengi kura 6 na Tobia Mahawe ambaye hakuwepo wakati wa zoezi la kuomba kura aliepata kura 4.
Katika nafasi hiyo hiyo, Sinorina Mongi alipata kura 1 na Pascal Athanas kura 3, kura zilizowanyima nafasi hiyo.
Nafasi ya Mweka hazina iliyokuwa inawaniwa na watu wawili ilienda kwa Steven Qamara aliepata kura 8 dhidi ya Sinorina Mongi ambaye hakupata kitu.
Mwenyekiti wa Kamati ya Uchaguzi ambaye pia ni Afisa Michezo mkoa wa Manyara Charles Maguzu na Fabian Manda Katibu wa Kamati na afisa Michezo Babati Mjini, Waliwataka viongozi hao waliochaguliwa kushirikiana na serikali katika kuendeleza mchezo wa riadha Manyara.
Pamoja na hayo afisa Michezo alitoa muda wa wiki moja kwa wale viongozi wenye kofia mbili katika uongozi kuachia nafasi moja na kutoa taarifa kwa maandishi.
Viongozi wapya wamepatikana wakati huu chama kikikabiliwa na madai kuwa wanariadha wengi wanaoshinda mashindano mbalimbali wanatoka Manyara lakini wameendelea kutangazwa kuwa wanatoka katika mikoa mingine.
No comments:
Post a Comment